 Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wakinyoosha mikono ili wapatiwe 
Rasimu ya Kanuni zitakazoendesha bunge hilo, juzi. Picha na Sulivan 
Kiwale
  
            
Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wakinyoosha mikono ili wapatiwe 
Rasimu ya Kanuni zitakazoendesha bunge hilo, juzi. Picha na Sulivan 
Kiwale
Endapo mapendekezo hayo yatapitishwa, hoja ya 
Katiba Mpya itakayowasilishwa na Kamati ya Bunge Maalumu la Katiba, 
itaamuliwa kwa kuungwa mkono na theluthi mbili ya wajumbe wa Tanzania 
Bara na idadi kama hiyo ya wajumbe kutoka Tanzania Zanzibar.
                
              
Upigaji kura huo kwa siri, umepongezwa na baadhi 
ya wabunge kwa maelezo kuwa utatoa fursa kwa wajumbe kupiga kura hizo 
kwa uhuru na bila kushinikizwa na misimamo ya vyama au taasisi 
zilizowapendekeza.
                
              
Kanuni hizo zimekuja wakati CCM, kikiwa 
kimewaagiza wajumbe wake ambao ndiyo wengi bungeni, kutetea muundo wa 
Serikali mbili badala ya ule wa Serikali tatu uliopendekezwa na Tume ya 
Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba.
                
              
Pamoja na CCM kuweka msimamo wa kuwataka wajumbe 
wake kuutetea mfumo huo, kumeibuka mgawanyiko mkubwa huku baadhi yao 
wakitarajiwa kukitosa na kuunga mkono mfumo wa Serikali tatu.
                
              
Kanuni ya 82(1) ya rasimu hiyo, imeweka bayana 
kuwa utaratibu utakaotumika kupata uamuzi baada ya mwenyekiti kulihoji 
Bunge ni wa ama kura ya siri au ya kielektroniki.
                
              
“Wakati wa kupiga kura ya siri, kila mjumbe 
atapiga kura ya Ndiyo au Hapana kwa kutumia karatasi za kupigia kura 
zitakazokuwa zimeandaliwa na Katibu wa Bunge,” inasomeka kanuni ya 
83(1).
                
              
Kanuni hiyo imeweka wazi kuwa kupiga kura kwa 
mujibu wa masharti ya kanuni hiyo, itakuwa ni wajibu na haki ya msingi 
ya kila mjumbe na kwamba kila mjumbe atapiga kura kwa binafsi yake.
                
              
Hatua ya wajumbe kupiga kura hiyo, itatanguliwa na
 kazi ya kila Kamati ya Bunge Maalumu, kujadili rasimu ya katiba hiyo 
kulingana na mgawanyo wa majukumu. Kamati 17 zitashughulikia ibara za 
rasimu.
                
              
Baada ya kukamilika kwa hatua hiyo, mwenyekiti wa 
Kamati ya Bunge ataagiza taarifa ya kamati iwekwe kwenye orodha ya 
shughuli kwa ajili ya kuwasilishwa bungeni kwa mjadala.
                
              
Kanuni hizo zimeeleza kuwa wakati wa mjadala huo, 
mjumbe yeyote anaweza kushauri na kutoa mapendekezo ya marekebisho au 
mabadiliko kwa ajili ya kuboresha sura ya rasimu inayohusika.
                
              
Hata hivyo, Kanuni za 78 (11) na 78 (12) za rasimu
 hiyo, zinapendekeza mwenyekiti asiruhusu hoja yoyote inayokiuka sheria 
au pendekezo la kamati linalohusu jambo lililo nje ya mamlaka ya Bunge.CHANZO MWANAINCHI
 
No comments:
Post a Comment