Saturday 15 February 2014

WAZIRI TIBAIJUKA AANIKA UTETEZI WA ZIWA NYASA...

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, ameweka wazi utetezi wa Tanzania katika mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa na Malawi.
Akizungumza na wahariri wa habari katika semina ya ardhi Dar es Salaam jana, Profesa Tibaijuka alisema tayari Rais Jakaya Kikwete ametoa ushahidi wa mpaka huo katika Kamati ya Marais Wastaafu, Festus Mogae wa Botswana, Joachim Chisano wa Msumbiji na Thabo Mbeki wa Afrika Kusini.
Katika ushahidi huo, kwa mujibu wa Profesa Tibaijuka, Tanzania ilitumia zaidi historia ya ugawaji mipaka ilivyokuwa na kutumia ushahidi wa nyaraka za serikali za kikoloni, zilizoshiriki kugawa mipaka ya Afrika.
Profesa Tibaijuka alisema mipaka ya nchi iliwekwa mwaka 1890 katika Mkataba wa Wajerumani waliokuwa wakitawala Tanganyika kwa kutumia hadithi za wagunduzi waliotangulia Afrika, kabla ya Wakoloni kuanza kugawana bara hilo.
Wakati huo kwa mujibu wa Profesa Tibaijuka, mpaka kati ya Tanganyika na Kongo na hata Malawi, ulikuwa Mashariki ya Ziwa na hivyo hata Ziwa Tanganyika, lilipaswa kuwa Kongo.
Alifafanua kuwa katika upimaji, baada ya kufanya uamuzi huo wa watawala, hatua ya pili ilikuwa kuunda tume kwenda kuhakiki mpaka huo kwa kuzungumza na wenyeji, na kuurekebisha kwa kufuata taarifa za wenyeji.
Mwaka 1898 tume hizo zikaundwa, na matokeo yake mipaka Ziwa Tanganyika, Mto Songwe na hata Ziwa Victoria ikawekwa katikati.
Kwa bahati mbaya, mwaka 1914 Vita ya Kwanza ya Dunia iliibuka na kusababisha tume hizo kusimama kazi kabla ya kupita na kuthibitisha mpaka katika Ziwa Nyasa.
Profesa Tibaijuka aliendelea kuanika ushahidi huo, kwamba baada ya vita ya dunia, Ujerumani ilishindwa na kupoteza makoloni yake ambayo yalichukuliwa na League of Nations ikiwamo Tanganyika ambayo ilitolewa kwa Uingereza kama mwangalizi.
Tanzania imethibitisha katika ushahidi wake kuwa, kitendo cha Uingereza kupewa Tanganyika kuwa mwangalizi huku Malawi ikiwa koloni lake, kilisababisha tume hiyo kutoendelea na kazi, kwa kuwa hakukuwa na umuhimu wa mpaka, wakati mtawala wa Malawi na Tanganyika akiwa mmoja.
Kwa mujibu wa Profesa Tibaijuka, Uingereza ilikuwa ikipeleka taarifa za uangalizi mara kwa mara League of Nations na kabla ya uhuru miaka ya 1950, Gavana wa Tanganyika alipeleka taarifa kutaka tume ifanye kazi yake kuhusu mpaka.
Profesa Tibaijuka alisema taarifa hizo ziko Geneva, Umoja wa Mataifa, na ujumbe wa Tanzania ulilazimika kwenda kupekua katika maktaba ya Umoja huo kupata vielelezo vya taarifa za Uingereza kuhusu mpaka, ambazo zimetumika katika ushahidi.
Ushahidi mwingine ambao Profesa Tibaijuka alisema utaisaidia Tanzania ni makubaliano ya kimataifa yaliyo chini ya Umoja wa Mataifa kuhusu kugawana eneo la maji.
Alisema kwa kufuata makubaliano hayo, haiwezekani watu wa Mbamba Bay, waombe kunywa maji ya Ziwa Nyasa kutoka Malawi

No comments: