| Rais wa Baraza Maaskofu Katoliki Tanzania, Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa | 
| Akisisitiza jambo | 
BARAZA
 la Maaskofu Katoliki Tanzania limewatoa hofu watanzania katika tamko 
lake lingine kwa Bunge Maalumu la Katiba (BMK) likisema haliko nyuma ya 
viongozi wala chama chochote cha siasa kama baadhi yao wanavyofiki.
Akitoa
 tamko hilo mjini Iringa jana, Rais wa Baraza hilo ambaye pia ni Askofu 
Mkuu wa Jimbo Kuu la Iringa, Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa alisema; 
“Baraza la Maaskofu Katoliki halina chama katika hili, lakini pia halina
 mtu au mwanasiasa au chama linachokifanyia kampeni kwa ajili ya 
Uchaguzi Mkuu wa mwakani.”
Katika
 Jubilei ya miaka 25 ya uaskofu wa Askofu Ngalalekumtwa iliyofanyika 
mjini Iringa hivi karibuni, Makamu wa Rais wa Baraza hilo, Askofu 
Severine Niwemugizi alitoa tamko kuhusu mchakato huo kwa kuwataka Umoja 
wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kurudi katika bunge hilo bila masharti.
April
 16, mwaka huu, wajumbe wanaounda umoja huo, waliamua kutoka nje ya 
bunge hilo wakipinga kile wanachosema ni kupuuzwa kwa makusudi maoni ya 
wananchi wanaotaka muungano wa muundo wa serikali tatu kama 
ilivyopendekezwa katika rasimu hiyo.
Katika
 tamko hilo Askofu Ngalalekumtwa alisema; “katika ujumbe wetu wa 
kichungaji wa Pasaka 2014, sisi maaskofu Katoliki Tanzania tuliwaandikia
 barua watu wote wenye mapenzi mema kwa nchi yetu tukiwaalika kuchukulia
 maanani mchakato wa kuandika katiba mpya.”
Alisema
 “wakati huu tunawaalika watanzania wote kwa pamoja, tuungane 
kuwakumbusha wale waliopewa dhamana ya kukamilisha Rasimu ya Pili ya 
Katiba kuwajibika binafsi na katika maridhiano kutupatia katiba 
maridhawa.”
Alisema
 wajumbe wa bunge hilo wanapasa kujadili kwa umakini kila kilichopo 
katika rasimu hiyo ili wafikie muafaka utakaoenzi ujasiri wa kipekee wa 
Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete wa kuanzisha 
mchakato huo.
“Tunawaasa tukiwaombea dhamiri zao zipate maoni mapya ili waweze kubeba kikamilifu dhamana hiyo waliyokabidhiwa,” alisema.
Askofu
 Ngalalekumtwa alisema baraza la maaskofu katoliki linawataka wajumbe 
 wa bunge hilo kuwa wamoja na kufanya kazi yao kwa mtazamo usioegemea 
siasa za vyama.
Alisema
 ni mategemo yao majadiliano yatafanyika kwa kuheshimiana, kutumia hoja 
za kizalendo na kiungwana na kuyaangalia kwa mapana mambo na masuala 
makuu yaliyopendekezwa katika rasimu hiyo.
“Kuandika
 katiba ni kazi iliyo ngazi ya juu zaidi ya siasa za vyama, na hivyo 
utashi wa kisiasa wa kuunda katiba mpya kwa kuzingatia Rasimu ya Pili 
utaweza kuridhiwa kwa kuzingatia msingi huu,” alisema.
Alisema
 kwa kadri nchi iliyivyo hivisasa kuna sababu za kutosha za kutaka 
Katiba mpya zikiwa ni pamoja na ufisadi, wananchi kujisikia kukosa 
usalama na amani, nchi kutokuwa na dira na tunu msingi.
“Na
 kwahiyo tunawasihi kwa mara nyingine tena ninyi wajumbe wa bunge hilo 
kurejea katika sehemu ya pili ya mjadala hapo mwezi Agosti mkiwa na moyo
 na mtazamo mpya,” alisema.
Alisema
 kwa kazi hiyo wajumbe hao watawasaidia watanzania waendelee kujivunia 
kuwa na taifa adilifu lenye amani na linalofanya kazi kwa pamoja kwa 
ajili ya manufaa na ustawi wa wote.
Alisema
 ikiwa matokeo yatakuwa yenye kuleta mema na kuimarisha amani na utulivu
 wa nchi, watanzania wote watawashukuru na kuwasifu na kama tunda la 
kazi ya bunge hilo litakuwa ni lenye kuingiza nchi katika matatizo 
zaidi, kuwataabisha wananchi na kukosa maelewano baina yao, basi 
watanzania watawahukumu na kuwawajibisha kwa kukosa umakini katika 
jukumu hilo muhimu mlilokabidhiwa.
Askofu
 Ngalalekumtwa alisema nchi haiko tayari kurudi nyuma na kuendelea na 
maisha yanayoongozwa na Katiba ya 1977 kwahiyo mahitaji ni kuwa na 
katiba itakayowezesha ushiriki kamili wa watu katika maamuzi na 
vipaumbele vya maendeleo ya Taifa.
“Tunataka
 Katiba ambayo inaruhusu utawala wa sheria, haki sawa kwa wote, manufaa 
na ustawi kwa wote na kuheshimu utu wa kila mmoja. Katiba shirikishi 
katika matumizi ya madaraka ili yatumike katika kuhudumia wote badala ya
 wachache na inayoweza kuzuia matumizi mabaya ya madaraka na ufisadi,” 
alisema.
Alipoulizwa
 msimamo wake nini kuhusu muundo wa serikali, Askofu Ngalalekumtwa 
alisema; “siwezi kusema popote pale, naogopa kuwapa ushawishi watu wetu 
na ndio maana msimamo wa kanisa ni kuwataka wajumbe wote warejee, 
wajadiliane na kutuletea katiba itakayokuwa na sifa hizo.”
 
No comments:
Post a Comment